YANGA SC YAAMBULIA POINTI YA KWANZA MICHUANO YA AFRIKA BAADA YA SARE YA 0-0
YANGA SC imepata pointi ya kwanza katika hatua ya makundi ya Kombe la Shirikisho la Soka Afrika baada ya sare ya bila kufungana na Rayon Sport ya Rwanda katika mchezo wa Kundi D uliofanyika Uwanja wa Taifa mjini Dar es Salaam. Kwa sare hiyo, Yanga inaendelea kushika mkia kwenye kundi hilo, nyuma U.S.M. Alger yenye pointi nne kileleni, Gor Mahia, Rayon pointi mbili kila moja baada ya mechi mbili za awali. Katika mchezo huo uliochezeshwa na marefa kutoka Angola, Helder Martins De Carvalho aliyepuliza filimbi akisaidiwa na washika vibendera Ivanildo Meirelles De O Sanche Lopes na Wilson Valdmiro Ntyamba, kwa mara nyingine udhaifu wa safu ya ushambuliaji ya Yanga uliiathiri timu. Yanga ilikuwa inacheza vizuri kuanzia nyuma ikipitisha mashambulizi yake pembezoni mwa Yanga, lakini mipira kila ilipofika mbele ilichukuliwa na wachezaji wa Rayon kwa urahisi. Winga chipukizi, Yusuph Mhilu ameendelea kuonyesha ubora wake kikosini Yanga, lakini nafasi zote alizotengeza hazikutumiw...